MAONO
Na. Kelvin Kitaso
sehemu ya Kwanza
“Pasipo maono watu hushindwa kujizuia”
Mithali 29:18
Maono ni kama kesho ya
mtu.Kesho ni siku ambayo hutarajiwa na
haijaonekana bayana bado, na hakuna mwanadamu yeyote chini ya jua aijuaye kesho
yake ipoje isipokuwa amejuzwa na Mungu ajuaye mambo yote kabla hayajatukia.
Kesho ni siku ambayo ni matokeo ya kile kitu ambacho kimefanyika leo; kesho
huandaliwa ndani ya leo, Mungu ndiye hutoa jawabu kama iwe kama vile
ulivyoiandaa.
Kuna msemo wa
kiingereza usemao, “Yesterday is history (jana ni historia), today is a gift
(leo ni zawadi), tomorrow is a mystery (kesho ni siri iliyofichika)” hii inaonyesha
kuwa katika maisha yote ya mwanadamu kuna siku tatu tu yaani jana, leo na kesho
na mwanadamu anapaswa kuzitumia siku zote hizo kwa faida yake mwenyewe na
kunufaisha jamii inayomzunguka pia.
Jana ni siku
ambayo imepita na hukutengenezea uzoefu (CV) ambao waweza kuwa mzuri au mbaya,
na kamwe hautoweza kurudi jana kuibadilisha jana yako ila unaweza kuitumia Leo
kuifanya kesho isijekuwa kama jana. Jenga tabia njema ya kutojisifia kwa mazuri
uliyofanya jana kwa kuwa kujisifia kutakufanya ujisahau kuwa unapaswa
kusababisha mambo makubwa kutokea tena na tena kamwe usijaribu kujilaumu kwa
vile ulivyoshindwa jana kwa kuwa itakufanya uwe muoga wa kujaribu kufanya mambo
makubwa leo. Lakini mazuri ya jana yanaweza kutumika kama marejeo kuwa kama
jana nilishinda basi na leo pia naweza kushinda kama ilivyokuwa kwa Daudi
aliporejea kuua simba na dubu pale alipotaka kupambana na Goliathi.
Kesho ni mimba
ambayo imetungwa leo na yapaswa kujifungua ni muhimu sana kuzingatia ili kuweza
kujifungua mtoto aliye mzuri na hii inatokana na mimba hiyo imetungwaje na
katika hali gani. Kujifungua mimba hii kunahitaji nguvu ya mbeba ujauzito na
pia Mungu akusaidie kujifungua salama.
Maono huweza
kuwa sawa na ahadi ambayo imetoka kwa Bwana kwa kuwa ahadi ni mambo yatarajiwayo
na hayajaonekana bayana bado, ufananaji wake unatokana na kuwa ahadi ya Mungu
huwa ni mambo ya kesho na ndiyo maana yanaitwa mambo yatarajiwayo na
hayajaonekana bado, na yakichanganywa na hakika pamoja na bayana ambayo ndiyo
imani hayabaki kuitwa maono au ahadi kwa kuwa tayari yametimia.
Kitu chochote unachokifanya leo kinaonesha kuwa
kesho yako itakuwaje.
|
Ni lazima uione
kesho yako ukiwa leo kwa kuwa kesho yako inategemea sana na wewe unaona nini
ndani yako mwenyewe ukiwa leo, na si kuona tu, pia unakiri nini kwa kuwa kuna
nguvu katika ukiri wa maneno, na si ukiri tu, bali ni nini ukifanyacho leo
kinaweza kuitimiza kesho yako. Kitu ukionacho ndani yako, ukikiricho na hata kukifanya
hugeuka kuwa tabia na kikiwa tabia mwishoni huja katika uhalisia wa utimilifu
wake.
Kesho yako
haitakuja kama muujiza yaani umeamka na kuiona tu inatimia, hapana ni mchakato
mrefu ambao unakuhitaji kutia juhudi za kutosha ili iingie kwenye utimilifu
wake. Kama haujaanza kuwaza kuwa kesho yako itakuja kuweje kamwe usijedhania
kama kitakuja kutimia kwako kitu ambacho hujawahi kukiwaza hata siku moja, mtu
anaweza kuhangaika na kitu ambacho amewahi kukiwaza hapo awali kuliko kile kitu
ambacho hajawahi kuwaza kabisa.
Kijana mmoja
alikuwa akisafiri kuelekea mahali asipopafahamu, baada ya kusafiri muda mrefu
akakuta sehemu kuna njia panda na akamuona mzee mbele yake katika hilo eneo,
akamuuliza Yule mzee nipite njia gani nifike sehemu ninayotaka kufika, Yule
mzee akamuuliza mahali anapotaka kuelekea ili amuelekeze njia ya kupita; kijana
akajibu kuwa hafahamu sehemu anayopaswa kwenda, Yule mzee akamwambia apite njia
yoyote kati ya zile azionazo au hata arudi alipotoka pengine anaweza kufika
mahali anapotaka kufika. Mfano huu ni sawa na mtu asiye na maono katika maisha
yake ni lazima awe mtu anayeshindwa kujizuia na hana muelekeo maalum.
Lazima uione
ndani yako kwanza. Mwanadamu huwa vile anavyowaza ndani yake kwa kuwa lile wazo
humpa hamasa ya kufanya kazi ili litokee na wazo pia la ndani yake huweza
kumfanya kukata tamaa ya kufika mbali. Mtu mmoja akasema kuwaza ni kuwaza tu
kama umewaza mambo makubwa au madogo ni bora ukawaza vitu vikubwa labda waweza
kuwa mtu mkubwa. Lakini kuwaza tu pasipo kuchukua hatua hakufai.
Mithali 23:7 “7
Maana aonavyo nafsini mwake, ndivyo alivyo.” Yaani ukitangulia tu kuona
kuwa wewe ni maskini mkubwa ni lazima uwe, ni lazima ujifunze kuona vyema. Watu
wakubwa duniani kabla ya kuwa vile walivyo, walitangulia kuona ukubwa ndani yao
kwanza na kisha wakaanza kufanya kazi kwa kuwa ile picha waliyoiona ndani yao
huwatesa kuifikia.
Katika biblia
neno ‘unaona nini?’ limeonekana mara saba na siku za wiki zipo saba, ina maana
ya kusema kila asubuhi BWANA huweza kukuuliza ‘unaona nini?’ mpaka zikaisha
siku saba za wiki na itakapoanza jumatatu ataanza na unaona nini? tena mpaka
Ijumaa huku akiunganisha na neno usiogope kwa kila siku uionayo katika uwepo
wako duniani.
Kofi Anan ambaye
ni katibu mkuu wa zamani wa umoja wa mataifa baada ya kuingia UN katika nafasi
ya kawaida tu akamwandikia mama yake ujumbe na kumtaarifu kuwa siku moja ni
lazima aje kuwa katibu wa umoja wa mataifa. Alivyoona ndivyo ilikuja kutokea na
kule kuona kwake kulimlazimu kutotulia na kuwa na juhudi kubwa sana ili baadae
aje kuwa katibu mkuu wa umoja wa mataifa.
Kama kuna picha
tayari unaiona ndani yako ya jinsi vile unavyopaswa kuwa ni muhimu sana
kuzingatia kuwa picha ile ni nguvu ya kukufanya upigane hata kuitimiza; ila
mbaya zaidi ni kwa mtu asiye na maono kwa kuwa hana picha ndani yake ni vigumu
kwa yeye kufanya kitu cha msingi.
Maandiko
yanasema katika Mithali 29:18 kuwa “18 Pasipo maono, watu huacha kujizuia”, tafsiri
ya asili ya kiebrania maono imetafsiriwa kama ‘hazon’ ambayo humaanisha mafunuo
ya neno la Mungu, na huendelea kwa kumaanisha kuwa pasipo neno la Mungu
kufunuliwa kwa watu ni lazima watu waende katika njia ya upotevuni. Mahali
popote ambapo neno la Mungu halijafunuliwa ni lazima watu waangamie na kuendelea
katika njia zao wenyewe kwa kuwa bado huwa kwenye mabano ya wafanye kipi na
kuacha kipi.
Kwa kuangalia
maono pia mtu yeyote ambaye hajafunuliwa ni maono gani alionayo ni kazi sana
kuwa katika njia sahihi. Jamii inayotuzunguka watu wengi hukosa maono na ndiyo
maana huishia kufanya vitu vya ajabu sana. Maono ni ile picha ya ndani aionayo
mtu kwa habari ya kesho yake na kama mtu haoni picha yoyote ndani yake ni
vigumu kufanya vitu vya msingi vya kimaendeleo.
Mtu mwenye maono
hata kama anaonekana maskini kwa wakati huo ni mtu wa tofauti kwa kuwa maono ni
muongozo wa utendaji kazi wa mtu huyo na ni lazima afanye mambo ambayo
yanapelekea utimilifu wa maono hayo na huishi maisha ya kujizuia katika mambo
yoyote ambayo hayamsaidii kufikia mwisho wake. Mtu mwenye maono hawezi kutulia
hata maono yake yawe yametimia.
Maono hutoa muongozo wa jinsi mtu apasavyo kuwa
na hata jamii ya kushirikiana nayo.
|
Nikiwa sehemu
fulani nahudumu baada ya huduma nikamuuliza kijana mmoja, je! Unataka kuja kuwa
nani? yule kijana akaniambia nataka kuja kuwa dereva na alikuwa anasoma, na
nilipomuuliza kwa nini anataka kuja kuwa dereva alieleza kuwa, ni kwa sababu
wazazi wake hawana uwezo wa kumuendeleza kimasomo, nilitafakari kuwa mtu huyu
anataka kuja kuwa dereva kwa sababu ya hali ngumu ya kiuchumi, ni vizuri ila
katika mazungumzo nikagundua kuwa amekata tamaa ya kufanikiwa zaidi kwa sababu
ya hali yake ila mwenye maono hata kama ana hali ngumu kamwe hataacha kuukiri
ushindi wake kuwa pamoja na ugumu uliopo ninaweza nikafika pale ninapokusudia
na hata kama nitachelewa kulingana na vikwazo vya hali niliyonayo sasa ila
nitahakikisha nimefika.
Pamoja na kuwa
mfanya kazi wa ndani kwa Potifa na kisha kupelekwa gerezani na kuwa mfungwa,
bado Yusufu aliendelea kuitazama na kuikiri ndoto yake ya kuja kuwa mtu mkubwa,
mazingira mabaya na ya kukatisha tamaa hayakumfanya Yusufu akate tamaa na
kubadilisha aina ya ndoto. Ni ukweli sana kuwa ugumu wa maisha ni sababu kuu
sana ya kusababisha watu kuyaacha maono yao ya uhalisia na kuingia katika
mengine ambayo si maono yao.
Mtu asiye na
maono ni lazima mambo yake yawe ovyo ovyo kwa kuwa hakuna mwongozo sahihi
unaoweza kumzuia asifanye yale ambayo anataka kufanya. Maono ni muongozo kwa
mtu mwenye nayo katika mambo yote na humuongoza kuwa sehemu sahihi kwa wakati
sahihi na kuwa na watu sahihi. Na ni nadra sana kumkuta mtu mwenye maono
anafanya mambo ambayo hayawezi kumsaidia kufikia utimilifu wa maono yake.
Ni muhimu
sana kwa mtu kuiona kesho yake ndani yake na aione katika uzuri ndipo anaweza
kutumia muda wake vizuri kutimiza yale ayaonayo. Kuona ni jambo jema sana ila
mtu anaweza kuogopa kuwaza mambo makubwa na hii hutokana na mtu kujidharau na
kuona kuwa ana uwezo mdogo sana ndani yake, hili ni tatizo la kiimani,
kutojitambua na kujidharau; ni lazima utoke kwenye eneo hili la kukosa
kujiamini na uanze kuona kuwa unaweza.
Maono makubwa, huleta taabu kubwa, (The greater
the revelation, the greater the tribulation)
|
Wakati fulani
nikiwa na rafiki yangu Christina akanena na kuniambia kwamba “the greater the
revelation, the greater the tribulation,” akimaanisha kuwa (maono makubwa
huambatana na taabu kubwa). Ukifuatilia kwenye biblia utaona kuwa watu wote
waliobeba maono makubwa ndio watu waliopata taabu kubwa hata utimilifu wa maono
yao. Usikate tamaa unapoona majaribu yamekuwa ni makubwa sana kwa upande wako,
kaa utulie huku ukitafakari kuwa ni uzito wa maono uliyonayo ndiyo sababu kuu
ya kuteseka kwako.
Mfano ni Mtume
Yohana aliyepata maono ya kitabu cha ufunuo akiwa katikati ya mateso makubwa na
kuwekwa katika kisiwa cha Patmo na Mtume Paulo ambaye alipata mateso makubwa
kulingana na ukubwa wa maono aliyokuwa amebeba.
itaendelea sehemu inayofuata...................
itaendelea sehemu inayofuata...................
Comments
Post a Comment