JESHI LA PEKEE LINALOWAUA ASKARI WAKE WALIOJERUHIWA NA KANISA LA YESU
KRISTO
Mwl: CARLOS RICKY WILSON KIRIMBAI
Mpendwa msomaji wangu unaweza ukawa
unakosea sana katika namna unavyoshughulika na mambo mbalimbali unayokutana
nayo maishani na ukajiona upo sawa tu.
Moja ya mahali ambapo unakuta
badala ya kumsaidia mtu aliyeharibu au kukosea tunammalizia kabisa ni Kanisani.
Ni ajabu sana umkute mtu amepata
shida au ajali na badala ya kumsaidia kwa kumkimbiza hospitalini au kumpa
huduma ya kwanza, wewe ukaamua kumalizia ili umwue kabisa.
Inakuwa mbaya sana pale unapoamini
kabisa kuwa unachofanya ni ibada kwa Mungu.
Kanisani hatuui watu kwa mapanga,
wala visu, mikuki wala mishale, hatuwaui kwa risasi bali kwa maneno.
Tunaua sifa zao na muonekano wao
katika jamii (character assasination).
Tunanukuu maandiko ya kuhalalisha
tukifanyacho huku tukiyasahau au kuyapuuzia kabisa maandiko yanayoagiza
vinginevyo.
Ndugu zangu, mtu akighafilika
katika kosa lo lote, ninyi mlio wa Roho mrejezeni upya mtu kama huyo kwa roho
ya upole, ukijiangalia nafsi yako usije ukajaribiwa wewe mwenyewe. (GAL. 6:1
SUV).
Hapa ni wazi kabisa kuwa mmoja wetu
akighafilika katika neno lolote walio wa Roho (sio tu kila mtu) wamrejeshe huyu
mtu kwa roho ya upole (sio maneno makali ya kushambulia facebook na insta na
kwenye mitandao ya jamii) na akituonya tuangalie sana nafsi zetu tusije
kujaribiwa sisi wenyewe.
Kosa la mwingine linaweza
kukupelekea ukosee kuliko huyo ambaye umebaki kujadili kosa lake na kumwita
kila aina ya majina yasiyo na staha au kiasi.
Tumeambiwa tujitahidi katika
upendano wa ndugu na upendano wa ndugu unafunika kosa na sio kulianika.
Kuchukiana huondokesha fitina; Bali
kupendana husitiri makosa yote. (MIT. 10:12 SUV).
Sio wivu wa nyumba ya Mungu ndo
unatusukuma kuanikana hadharani bali ni chuki tuliyo nayo moja kwa mwingine ndo
inatupelekea kuanikana hadharani na wivu tuliyo nao mmoja kwa mwingine.
Haiwezekani kuanguka kwa mmoja wetu
badala ya kuwa msiba kwetu ndo inakuwa sherehe kwetu.
Tumekuwa kuwa kama ndege wala
mizogo (vultures).
Tumekuwa kama fisi wala mizoga. Kwanini
tunafurahia kula mizoga ya wengine?
Kwanini tunajilisha na makosa ya
watu wengine? Au labda inatufanya kwa muda tuyasahau ya kwetu wenyewe?
Upendo siku zote utatusukuma
kusitiri makosa ya wengine.
Zaidi ya
yote iweni na juhudi nyingi katika kupendana; kwa sababu upendano husitiri
wingi wa dhambi. (1 PET. 4:8 SUV).
Juhudi katika kupendana sisi kwa
sisi kutatupelekea tuwe wepesi zaidi kusitiririana kuliko kuanikana.
Sasa mmoja
anaweza kusema ina maana tuunyamazie upuuzi ambao unafanyika kati yetu?
La hasha.
Lakini sio
kwa kuanikana na kudhalilishana hadharani.
Mungu katuwekea utaratibu mzuri wa
kushughulika na mambo yetu.
Tukumbuke kuwa kanisa ni la Mungu
hata hivyo na sio letu na Yeye Ndiye anaweka utaratibu wa kushughulika na vitu
miongoni mwetu.
Na ameshasema walio wa Roho kati
yetu wamrejeshe sio kumtenga, kumsema, kumsengenya na kumshambulia huyo mtu.
Ameshasema tusitiri wingi wa makosa
na sio kuanika.
Ameshasema tusitiriane.
Maandiko yanasema:
Usiende huko na huko katikati ya
watu wako, kama mchongezi; wala usisimame kinyume cha damu ya jirani yako; mimi
ndimi BWANA. Usimchukie ndugu yako moyoni mwako; ni lazima kumkemea jirani
yako, wala usichukue dhambi kwa ajili yake. Usifanye kisasi, wala kuwa na
kinyongo juu ya wana wa watu wako; bali umpende jirani yako kama nafsi yako;
Mimi ndimi BWANA. (LAW. 19:16-18 SUV).
Ona maandiko yalivyo wazi.
Anatuambia tusiende huko na huko
katikati ya watu wa Mungu kama wachongezi wala tusisimame kinyume na damu ya
jirani zetu.
Tusiwamalizie watu ambao tayari
wanatokwa damu kwa sababu ya makosa ambayo wameyafanya.
Tusimchukie jirani bali tumkemee
ili tusije tukabeba dhambi kwa ajili yao lakini huko kukemea kusifanyikie
hadharani na tusifanye kama kisasi au kwa kinyongo dhidi ya mwenzako.
Nimalizie kwa andiko ambalo
linatusaidia kuelewa nini maana ya kufunika dhambi au kusitiri makosa.
Sio kuipotezea bali hasa namna
tunavyoshughulika nayo.
Ndugu zangu, ikiwa mtu wa kwenu
amepotelea mbali na kweli, na mtu mwingine akamrejeza; jueni ya kuwa yeye
amrejezaye mwenye dhambi hata atoke katika njia ya upotevu, ataokoa roho na
mauti, na kufunika wingi wa dhambi. (YAK. 5:19-20 SUV).
Ameiweka wazi sana kuwa miongoni
mwetu mtu akiwa amepotelea mbali na kweli yaani anafanya vitu kinyume na Kweli
mtu mwingine amrejeze, sio ndo tunamsukumia mbali kabisa kwa namna tunavyo
ihandle situation yake.
Tunapomrejeza mkosaji au mwenye
dhambi hata atoke katika njia yake ya upotevu tutakua tunaiokoa roho na mauti
na kufunika uwingi wa dhambi.
Kwa hiyo kama unachofanya
hakimrejezi huyo mtu uwe na uhakika unachofanya kinamwua huyo mtu na ndo maana
nikatangulia kusema jeshi la pekee linaloua majeruhi wake ni Kanisa la Yesu.
Mbaya zaidi ni pale tunapoona tupo
sawa katika tunachofanya kwa kunukuu maandiko nje ya muktadha.
Kinachoathiri Kanisa sio makosa
yanayofanywa bali namna tunavyoshughulika na hayo makosa yaliyofanywa.
Yesu alisema amri mpya anatuachia.
Tupendane sisi kwa sisi kama Yeye
alivyotupenda.
Je tunapokosea Yeye huwa
anatuanika?
Anaweza kufanya hivyo mjue!
Anasema tukipendana kama
alivyotupenda watu wote watajua kuwa sisi ni wanafunzi Wake.
Ndo maana wanashindea kujua kama
sisi ni wanafunzi Wake kwa sababu tunachukiana sana na kuwekeana visasi balaa.
EE MWENYEZI MUNGU TUREHEMU.

Ukweli mtupu
ReplyDelete